Lugha Nyingine
Afrika CDC yapongeza uzinduzi wa kampeni ya chanjo dhidi ya mpox nchini DRC
Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kukinga Magonjwa (Afrika CDC) kimeipongeza Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kwa kuzindua vyema kampeni yake ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa mpox katika majimbo mawili yaliyopewa kipaumbele.
Katika taarifa ya Jumapili, CDC Afrika imesema kuwa uzinduzi huo unaashiria hatua muhimu katika juhudi zinazoendelea za kudhibiti mlipuko wa mpox na kulinda makundi ya watu walio hatarini kote nchini humo.
Huku ikibainisha uungaji wake mkono kwa juhudi za DRC kukabiliana na ugonjwa huo, hususan utoaji chanjo kwa makundi yaliyo hatarini katika majimbo ya Equateur na Kivu Kaskazini nchini humo sambamba na washirika wengine wa kimataifa, CDC Afrika imesema kampeni hiyo ya chanjo itafanyika pia kwenye majimbo mengine hivi karibuni ili kuhakikisha upatikanaji jumuishi zaidi.
Wiki iliyopita, CDC Afrika ilibainisha kuwa idadi ya jumla ya wagonjwa wa mpox barani Afrika imeongezeka na kufikia 34,297, ikiwemo maambukizi 6,806 na vifo 866 vilivyothibitishwa tangu kuanza kwa mwaka huu, huku DRC ikiwa kitovu cha mlipuko wa sasa wa ugonjwa huo barani Afrika.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma